WALIMU WAKUU 284 SHULE ZA MSINGI WAPATIWA MAFUNZO UTHIBITI UBORA



Na Shushu Joel Bagamoyo

"Elimu Bora kwa Maendeleo Bora" ni kauli mbiu inayoibeba taasisi ya Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu (ADEM) iliyopo Bagamoyo Mkoani Pwani iliyojikita katika utoaji Mafunzo ya Uongozi kwa Walimu Nchini. Katika kuhakikisha na kusimamia hilo, Wakala umeendesha

Mratibu wa mafunzo ya uthibiti ubora shule za msingi Bi, Evodia Marco akisoma taarifa ya mafunzo mbele ya mgeni rasmi wakati wa ufungaji wa mafunzo hayo(NA SHUSHU JOEL)


Mafunzo maalum ya Uthibiti Ubora wa Shule wa ndani kwa Walimu wakuu 284 kutoka Mkoa wa Pwani yaliyofanyika kuanzia tarehe 13/04/2021 na kufungwa rasmi tar 15/04/2021 na Afisa Elimu Mkoa wa Pwani, Bi. Hadija Mcheka, katika Kampasi ya Wakala iliyopo Bagamoyo Mkoani Pwani.

 

Mafunzo hayo yalijikita katika kuwajengea uwezo Walimu Wakuu katika maeneo ya

Uthibiti Ubora wa Shule, Ubora wa Mtaala katika kukidhi mahitaji ya Mwanafunzi, Mafanikio ya Mwanafunzi, Ubora wa Ujifunzaji na Upimaji mzuri, Ubora wa Utawala ktk Uongozi wa Shule, Ubora wa mazingira na athari yake katika kuboresha ustawi, Afya na Usalama wa Wanafunzi, Ufuatiliaji na tathmini ya Uthibiti ubora wa Shule wa ndani.

 

Afisa Elimu Mkoa wa Pwani Bi. Hadija Mcheka aliyekuwa Mgeni rasmi katika ufungaji wa mafunzo hayo ameipongeza ADEM kwa kuratibu na kuendesha mafunzo hayo, yaliyoandaliwa kwa weledi ili kutatua changamoto za usimamizi wa utoaji huduma bora za elimu katika Shule za Msingi katika Mkoa wa Pwani.

" Nimefarijika sana kuona Walimu Wakuu wa Mkoa wa Pwani ninaousimamia wamepewa kipaumbele katika kupatiwa mafunzo haya hivyo ni lazima Walimu Wakuu mlioshiriki mafunzo haya mtambue kwamba mna wajibu wa kuhakikisha shughuli ya utoaji wa elimu katika Shule zetu za Msingi, zinatekelezwa kikamilifu na kwa moyo ili watoto wetu waweze kupata elimu bora na si bora elimu" Amesema Bi. Hadija Mcheka.

Baadhi ya walimu wakuu kutoka shule za msingi mbalimbali wilayani Bagamoyo wakifuatilia kwa makini hotuba mbalimbali zilizokuwa zikiytolewa siku ya mwisho ya mafunzo

Anaongeza kusema, nina imani kuwa mafunzo haya yamewaongezea umahiri katika uongozi, kusimamia, kufuatilia na kutathimini utekelezaji wa maelekezo ya Serikali ya kutoa huduma ya elimu vile inavyopaswa kwani tumekua na miongozo mbalimbali ya Serikali inayotuongoza katika kusimamia na kutekeleza majukumu yetu, lakini pamoja na miongozo hiyo na nyaraka mbalimbali bado tunahitaji kupata mafunzo kama haya yaliyoendeshwa hapa ili kuboresha utendaji kazi wetu.

 

Akifafanua zaidi Bi. Hadija Mcheka amesema, nia ya Serikali yetu ni kuendelea kuboresha mazingira ya utoaji wa elimu katika taasisi za elimu ikiwemo Shule za Msingi kama ilivyofanya katika kuhakikisha mnapatiwa mafunzo haya.

"Nitumie fursa hii kuwakumbusha walimu Wakuu wa Mkoa wa Pwani kwenda kuyafanyia kazi maeneo yote ambayo yamefundishwa katika siku zote tatu za mafunzo, mkatumie vizuri fursa hii ya mafunzo katika kuimarisha uongozi na ufundishaji katika Shule zetu kwani kwasasa tunahitaji Uongozi bora unaoleta matokeo chanya na Uongozi unaoacha alama katika sekta ya Elimu Nchini"

 

Akimalizia hotuba yake ya ufungaji mafunzo hayo, Bi Hadija Mcheka, ametoa rai kwa Walimu Wakuu wa Mkoa wa Pwani waliopatiwa mafunzo hayo kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali za kutoa elimu bora, ili kuzalisha wahitimu waliosheheni maarifa na ujuzi, unaowawezesha kushiriki katika shughuli mbalimbali za maendeleo na kuahidi kuwa

Mkoa utaendelea kuitumia ADEM katika mafunzo ya Uongozi na Usimamizi wa elimu na kufanya ufuatiliaji katika Shule za Msingi kuona kama Walimu Wakuu waliopokea mafunzo haya wanayatumia kuleta mabadiliko na matokeo chanya katika maeneo yao.

 

Nae Kaimu Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Maendeleo ya Elimu (ADEM), Dkt. Alphonce Amuli akizungumza katika ufungaji wa mafunzo hayo, amewashukuru walimu Wakuu 284 kutoka Halmashauri 8 za Mkoa wa Pwani walioitikia wito wa kuhudhuria mafunzo hayo na kuwataka kuyatumia kama chachu ya kwenda kuimarisha usimamizi na ufuatiliaji wa utolewaji wa elimu bora katika vituo vyao.

 

Kwa kipindi kirefu mfumo wa uthibiti ubora wa Shule wa ndani umekua na changamoto za kiuongozi, zilizopelekea Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kuona umuhimu wa kufanya maboresho ya mifumo hiyo kwa kufanya mafunzo haya ya Uthibiti Ubora wa ndani wa Shule kwa Walimu wakuu, mafunzo yaliyofadhiliwa na mradi wa GPE-LANES II na kuratibiwa na kuendeshwa na Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu (ADEM), hii ikiwa ni awamu ya pili ya utoaji wa mafunzo hayo yaliyotolewa kwa Walimu Wakuu 284 katika Mkoa wa Pwani, 210 kutoka Mkoa wa Songwe na 196 kutoka Mkoa wa Dar Es Salaama huku awamu ya kwanza ya mafunzo hayo ikiwa imefanyika Mwezi Januari kwa kutoa mafunzo ya Uthibiti Ubora wa Shule wa ndani kwa Walimu Wakuu wa Shule za Msingi 8,091 wa Tanzania bara.

MWISHO

Post a Comment

0 Comments