NA MWANDISHI WETUI
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Mhe. Stanslaus Nyongo (Mb) ameushauri uongozi wa Chuo Kishiriki cha Elimu Mkwawa (MUCE) kujikita kutangaza fursa hasa za Shahada za Umahirii ili kuongeza mapato ya ndani ya chuo hicho.
![]() |
Picha ya pamoja ya viongozi mbalimbali |
Ameyasema hayo mkoani Iringa mara baada ya Kamati hiyo kukagua Mradi wa ujenzi wa Maabara ya Kemia na ya Viumbehai zinazojengwa katika chuo hicho na kuongeza kuwa mapato hayo yanaweza kutumika kujenga mabweni yatakayosaidia kupunguza changamoto hiyo.
"Nimeona katika taarifa yenu mna idadi ndogo ya wanafunzi wa Shahada za umahiri, inabidi mfanye jitihada kubwa kukitangaza chuo hasa katika Shahada hizo ambazo zina idadi ya wanafunzi wachache ili kujiongezea mapato ya ndani," amesema Mhe. Nyongo.
Katika hatua nyingine Mhe. Nyongo pia ameitaka Wizara ya Elimu kufuatilia suala la kukiboresha kukipandisha hadhi Chuo cha Ualimu Mtwara ili kitumike kuzalisha walimu watakaofundisha katika Shule za Sekondari nchini.
"Tumejenga shule nyingi kipindi hiki na tuna upungufu wa walimu, nashauri Wizara ifuatilie suala la kuwa na Chuo Kikuu katika mkoa wa Mtwara ambalo limeshaongelewa hata bungeni ili tuweze kuzalisha walimu wengi watakaopunguza changamoto ya upungufu wa walimu katika Shule za Sekondari," amesema Mhe. Nyongo.
"Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. Omari Kipanga (Mb) amesema Wizara imepokea mapendekezo yote yaliyotolewa na Kamati hiyo na kuahidi kwenda kuyafanyia kazi kwa kushirikiana na Taasisi husika hasa katika kujitangaza".
Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa James Mdoe amesema Serikali imepokea mkopo wa Dola milioni 425 kupitia Mradi wa HEET zitakazotumika kuboresha Vyuo na Taasisi za Umma za Elimu ya Juu ambapo Chuo cha MUCE kitapatiwa Dola milioni 8 kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya chuo hicho.
0 Comments